Saturday 21 October 2017

LISSU ATOLEWA ICU, AFYA YAIMARIKA


AFYA ya Mbunge wa Singida Mashariki (CHADEMA), Tundu Lissu, imeimarika na sasa ameondolewa kwenye Chumba cha Wagonjwa Mahututi (ICU), katika hospitali anayotibiwa ya Aga Khan, jijini Nairobi, nchini Kenya.
Hayo yalisemwa jana na Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, alipozungumza na vyombo vya habari, kuhusu hali ya afya ya Lissu, ambaye alishambuliwa kwa risasi nyumbani kwake, Dodoma.
Mbowe alisema, Lissu alitoka ICU, wiki iliyopita, ambako alikuwa akipatiwa matibabu ya kuondolewa risasi katika mwili wake.
“ Kwa sasa Mheshimiwa Lissu ametoka ICU, baada ya kufanyiwa upasuaji mara 17 mpaka sasa. Mashine zilizowekwa katika mwili wake zimeondolewa.
“Sasa hivi hatumii mipira ya oksijeni, hatumii mipira ya chakula na anakula mwenyewe bila ya kutumia mipira,”alisema .
Alisema kwa sasa,  Lissu anaweza kukaa mwenyewe, huku akitembelea kiti cha kusukuma na kwamba, mwishoni mwa wiki, alitembezwa katika baadhi ya maeneo ya karibu ya jiji hilo ili kupata hewa safi.
Alisema kutokana na hali yake kuimarika, picha zake na pamoja na anavyozungumza, zitaanza kurushwa katika mitandao ya kijamii, ili jamii iweze kumuona hali yake.
“Kuanzia leo (jana), mtaanza kusikia sauti yake na kuiona video yake, tulikataa kutoa picha zake zaidi ya mwezi, lakini kwa sasa tutatoa,”alisema.
Akizungumzia matibabu yake, alisema  mpaka sasa  yako katika awamu ya pili katika hospitali hiyo, ambapo ya kwanza yalifanyika katika Hospitali ya Rufaa ya Mkoa wa Dodoma.
Alisema awamu ya tatu ya matibabu yake, itafanyika hospitali nyingine nje ya Kenya, kwa ajili ya kuendelea na matibabu zaidi.
Hata hivyo, alisema kwa sasa hospitali na nchi anayokwenda kutibiwa hawawezi kuitaja kutokana na sababu za kiusalama.
Alisema kabla ya mwisho wa mwezi huu, wanatarajia mbunge huyo kuruhusiwa,  iwapo madaktari wa hospitali hiyo wataridhika na afya yake.
Kuhusu  waliochangia gharama za kumtibia Lissu, aliwashukuru wananchi bila ya kujali itikadi za vyama, serikali na wadau nje ya nchi, kwa kuchangia gharama za matibabu hayo.
Septemba 7, mwaka huu, Lissu alipigwa risasi na watu wasiofahamika, wakati akirejea nyumbani kwake, baada ya Bunge kuahirishwa nyakati za mchana.

000000000

No comments:

Post a Comment