Thursday 19 November 2015

SERIKALI YATOA SIKU 30 KWA WASIOENDELEZA VIWANDA NA MASHAMBA




NA MWANDISHI WETU
SERIKALI imetoa siku 30 kwa wawekezaji waliowekeza kwenye viwanda na mashamba yaliyokuwa yakimilikiwa na serikali, kuwasilisha taarifa za utekelezaji wa mauzo baada ya baadhi yao kushindwa kuviendeleza.
Imesema endapo wawekezaji hao watashindwa kutoa taarifa hizo za utekelezaji wa mikataba, viwanda na mashamba hayo yatarejeshwa serikalini.
Hatua hiyo ni sehemu ya mpango wa kuvirejesha viwanda na mashamba ambayo wawekezaji wake kushindwa kutekeleza mpango wa uwekezaji kwa kuvibadilishia matumizi.
Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa jana na Msajili wa Hazina, Lawrence Mafuru, alisema ofisi hiyo inapitia mikataba yote ya ubinafsishwaji wa viwanda na mashamba.
Alisema wapo baadhi ya wawekezaji wamekiuka masharti ya mikataba hiyo, ambapo baadhi wamechukua mashine kwenye viwanda na mashamba bila kuzirejesha mashine mbadala.
Alibainisha kuwa masharti mengine yaliyokiukwa ni baadhi ya viwanda na mashamba kubadilishiwa matumizi kinyume na mikataba na kutokukamilisha malipo ya ununuzi.
Msajili huyo wa hazina aliwataka wawekezaji walionunua mali hizo zilizokuwa zikimilikiwa na serikali, kuwasilisha taarifa zao za utekelezaji wa mikataba ya mauzo serikalini ndani ya siku 30.
Endapo wawekezaji hao watashindwa kutekeleza maagizo hayo ya serikali, Mafuru alisema hatua stahiki zitachukuliwa, ikiwemo kurejesha viwanda na mashamba hayo kwenye miliki ya serikali.
Maamuzi hayo ya serikali ni muendelezo wa utekelezaji wa ahadi za Rais Dk. John Magufuli, ya kurejesha viwanda  na mashamba yaliyokuwa yakimilikiwa na serikali ambayo wawekezaji wameshindwa kuyaendeleza.
Alipokuwa akiwahutubia wananchi kwenye mikutano ya kampeni kabla ya kuchaguliwa kuwa Rais, Dk.Magufuli alisema mara atakapopata ridhaa ya Watanzania, atarejesha serikalini viwanda vyote vilivyobinafsishwa bila kuendelezwa.
 Alisema hatua hiyo itakwenda sambamba na ufufuaji wa viwanda na kujenga viwanda vingine ili kuondoa tatizo la ajira kwa vijana.

No comments:

Post a Comment