Wednesday 3 August 2016

JPM: CCM INA UWEZO WA KUTAWALA MILELE




MWENYEKITI wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), Rais Dk. John Magufuli, amesema licha ya wapinzani wachache kutaka kukwamisha utendaji wake wa kazi na utekelezaji wa Ilani ya Chama, CCM itaendelea kutawala Tanzania.
Amesema uwezo inao wa kutawala milele, inakubalika kwa wananchi na kuwaomba wanachama wapya anaowaita ng’ombe waliokatika ‘mikia’, wanaotaka kurudi zizini la CCM mkoani Geita, wamsubiri atakapofanya ziara ya kichama.
Rais Magufuli alisema hayo juzi, kwenye uwanja wa Kalangalala, wakati akihutubia maelfu ya wananchi waliofika kumlaki na kumsikiliza alipokuwa akitokea mkoani Shinyanga.
“Wana-CCM wote waliopo hapa na wengine wote, nawashukuru kwa kunichagua, niko pamoja nanyi na sitowaangusha. Changamoto zilizoko kwenye Chama tutazishughulikia na kuzitatua pamoja,” alisema na kushangiliwa.
Aliamsha tena shangwe alipovikejeli vyama vya upinzani, kikiwemo kinachopanga kufanya vurugu kwa kuandamana, akisema: “CCM itaendelea kutawala milele, uwezo inao na inakubalika kwa wananchi.
Wale wasio na mikia, wanaotaka kuhamia na kurudi tena CCM, wasubiri nikija nimevaa kijani.”
Mwenyekiti huyo mpya wa CCM alisema hayo kufuatia sauti za baadhi ya wananchi waliokuwa wakidai wanataka kurudisha kadi za vyama uchwara ili wachape kazi, baada ya kuruhusiwa kupatiwa mawe yenye mabaki ya dhahabu, maarufu kwa jina la ‘Magwangala’.


Ahadi ya kujenga kilometa 10 za lami Geita iko palepale
RAIS Dk. John Magufuli amesema serikali itajenga barabara  yenye urefu wa kilometa 10 za lami katika mkoa wa Geita, ikiwa ni moja ya utekelezaji wa ahadi alizozitoa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu wa mwaka jana, kwa wananchi wa mkoa huo.
Aidha, amesema barabara ya Kahama- Geita, ambayo upembuzi yakinifu na usanifu umekamilika, nayo itajengwa kwa kiwango cha lami.
Rais Magufuli alisema hayo juzi, mjini hapa, wakati akihutubia maelfu ya wananchi wa Geita katika uwanja wa Kalangalala.
Aliwataka wananchi wasing’ang’anie matuta ya barabarani na kudhani ndiyo suluhisho la mwisho la ajali za barabarani.
“Kilometa kumi za lami nilizoahidi, tutazijenga. Mheshimiwa Kanyasu na wenzake wakae wapendekeze zijengwe wapi, lakini wananchi msing’ang’anie matuta, hatuwezi kujenga barabara ikajaa matuta, ingekuwa hivyo gari zingekuwa zinapita hata kwenye matuta ya viazi,” alisema.
Alisema waendesha pikipiki (bodaboda) ni moja ya chanzo cha ajali, wakigongwa au kugonga wanasema ‘weka matuta’,  hivyo ni vyema kila mtumiaji wa barabara akatimiza wajibu wake kwa kufuata sheria za barabarani.
“Barabara nyingine ya Kahama-Geita, upembuzi wake umekamilika na tumetenga shilingi milioni 400, kwa ajili ya ujenzi wa barabara hiyo,” alisema.
Hata hivyo, alisema barabara zilizoahidiwa kupandishwa hadhi zitapandishwa, ambapo aliwaomba wananchi waendelee kumuamini kwani atasimamia vyema Ilani ya Uchaguzi ya CCM.
Rais Magufuli alilipongeza Jeshi la Polisi, Kikosi cha Usalama Barabarani kwa kudhibiti ajali nyingi, kupambana na vitendo mbalimbali pamoja na kudhibiti matukio ya uhalifu.
Awali, mbunge wa Jimbo la Geita Mjini, Costantine Kanyasu, alimuomba Rais Magufuli awapatie wananchi mabaki ya mawe yenye dhahabu, maarufu kwa jina la Magwangala.

No comments:

Post a Comment